Idara ya upelelezi nchini DCI imetoa arifa ya watu wanane wanaotafutwa ambao wamepewa mafunzo ya hali ya juu, wamejihami na ni washukiwa hatari wa ugaidi ambapo baadhi yao wana uhusiano na kundi la kigaidi la Al Shabaab.
Mkurugenzi wa upelelezi,George Kinoti, amehimiza uma kutoa habari zozote zitakazosaidia kukamatwa kwa washukiwa hao.
Washukiwa hao ni pamoja na Mohamud Abdi Aden anayefahamika kwa jina lingine kama Mohamed Yare kutoka kauntyi ya Garissa,Abdikadir Mohamed Abdikadir anayefahamika kwa jina lingine kama Ikrim, Ahmed Ali Mohamed na Mohamed Ali Hussein, Kassim Musa Mwarusi, Peter Gichungu Njoroge, Erick Njoroge Wachira na Abdurahman Hija.
Kulingana na maafisa wa upelelezi, Mohamed Ali Hussein pamoja na Ahmed Ali Mohamed, walikuwa sehemu ya shambulizi lililotibuka la Al-Shabaab la mwaka 2018.
Idara ya DCI ilisema Abdurahman Hija almaarufu Mnubi na Erick Njoroge Wachira almaarufu Mohamed, walikuwa sehemu ya genge ambalo lilikuwa likiwahangaisha wakazi wa Nyeri.
Abdikadir Mohamed Abdikadir amehusishwa na kundi la kigaidi la Al-Qaeda lenye makao yake nchini Yemen. Alihusika katika lile shambulizi la Dusit mwaka 2019 na mlipuko wa bomu wa Kampala mwaka 2010.
Peter Gichungu ambaye ni mwanafunzi wa zamani wa chuo kikuu cha JKUAT, alitiwa nguvuni mjini Mandera alipokuwa akielekea kujiunga na Alshabab.
Alishtakiwa na baadaye Kuachiliwa huru tarehe sita mwezi Machi mwaka 2020, na baada ya kukaa hapa nchini kwa muda mfupi, alisafiri nchini Somalia kujiunga na Alshabab akiandamana na mpenzi wake wa kike Miriam Hamisi.
Idara ya DCI inaamini kuwa washukiwa hao ambao wamejihami na wametajwa kuwa hatari, wamo humu nchini kutekeleza mashambulizi ya kigaidi.
Mkurugenzi wa idara ya DCI George Kinoti ametoa wito kwa umma kutoa habari zozote zitakazosababisha kukamatwa kwa washukiwa hao.