Mabondia wanne wa Kenya watashuka ulingoni mjini Istanbul Uturuki , kwenye mashindano ya dunia kwa wanawake ,baada ya wanamasumbwi wawili kubanduliwa katika raundi ya mchujo.
Teresia Wanjiru atapigana na Mwitaliano Confora Assunta katika pigano la uzani wa Light Welter raundi ya 32.
Katika pigano la raundi ya 32 bora uzani wa Fly,Ann Wanjiru atapimana ubabe na Kobb Tettiana wa Ukraine akiwa bondia wa pili wa kikosi cha Hit Squad kuchuana na mpinzani wa Ukraine .
Beatrice Akoth atarusha makonde dhidi ya Romeu Jocielen wa Brazil katika raundi ya 32 bora uzani wa feather huku Elizabeth Akinyi akizichapa na Makno Karolina wa Ukraine raundi ya 32 bora uzani wa kadri.
Christine Ongare alikuwa bondia wa pili wa Kenya kuyaaga mashindnao baada ya kupigwa alama 5-0 na Hanna Okhato wa Ukraine Jumanne jioni uzani wa chini zaidi , na awali Lorna Kusa alipoteza kwa Khalzova Valentine wa Kazakistan katika raundi ya 32 bora uzani wa light middle.
Kenya inawakilishwa na wanamasumbwi 10 kwenye mashindano hayo ya dunia,wakiyatumia kujiandaa michezo ya jumuiya ya madola itakayoandaliwa mjini Birmingham Uingereza kati ya Julai na Agosti mwaka huu.