Rais Uhuru Kenyatta amewahakikishia wakenya kwamba ujenzi wa bwawa la Thwake utakaogharimu mabilioni ya pesa, utakamilika mwezi june mwaka ujao.
Akiongea wakati wa ukaguzi wa mradi huo kwenye kaunti ya Makueni, Rais Kenyatta aliagiza halmashauri ya kuhifadhi mazingira ya NEMA kuzindua mara moja kazi ya kuusafisha mto Nairobi na mito nyingine ili kuhakikisha kwamba maji yatakayo tiririka kwenye bwawa la Thwake ni salama kwa matumizi ya binadamu.
Kiongozi wa taifa alisema kuwa bwawa hilo la Thwake litakuwa afueni kubwa kwa wakazi wa kaunti za Makueni na Machakos ambao wamekuwa wakikumbwa na tatizo la muda mrefu la uhaba wa maji.
Mradi huo ambao ni miongoni mwa Miradi ya ruwaza 2030 unatarajiwa kukamilika kufikia mwezi Juni mwaka 2022.
Kiongozi huyo wa taifa pia anatarajiwa kuzuru Jiji la Konza, kuzindua barabara ya Kibwezi-Kitui pamoja na jumba la mikutano la Machakos.
Rais Uhuru Kenyatta alilakiwa na mawaziri kadhaa wakiongozwa na Monicah Juma, kiongozi wa ODM Raila Odinga, kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka, magavana wa eneo la Ukambani Charity Ngilu, Alfred Mutua, Kivutha Kibwana na Seneta wa Makueni Mutula Kilonzo miongoni mwa wengine.
Ziara hiyo imejiri siku kadhaa baada ya Rais Uhuru Kenyatta kuahirisha ziara hiyo akitaja ongezeko la visa vya Covid-19.
Hapo awali msemaji wa Ikulu Kanze Dena alipuuzilia mbali madai kwamba Rais alifutilia mbali ziara hiyo kutokana ubabe wa uongozi miongoni mwa viongozi wa ukambani.