Serikali ya kaunti ya Garissa kwa ushirikiano na shirika la msalaba mwekundu zimeweka vituo vinne vya kupima virusi vya Covid-19 katika eneo hilo.
Naibu mkurugenzi wa huduma za matibabu Ahmed Bashey alisema vituo hivyo vya kupima corona vilivyoko katika gereza la Garissa, shule ya msingi ya Garissa na hospitali ya rufaa sasa vinafanya kazi na viko tayari kwa wananchi wanaotaka kupimwa virusi hivyo.
Akizungumza katika kituo cha kupima covid-19 kilichoko katika shule ya msingi ya Garissa, Bashey aliwahimiza wakazi wa eneo hilo kutembelea vituo hivyo kwa upimaji wa covid-19 bila malipo.
Kwa mujibu wa Bashey serikali ya kaunti ya Garissa imechukua hatua hiyo kufuatia visa vinavyoongezeka vya Covid-19 miongoni mwa wakazi wa sehemu hiyo.
“Katika muda wa saa 72 zilizopita, tumethibitisha visa 5 vipya na hivyo kufikisha idadi jumla ya visa vya Corona katika kaunti ya Garissa kuwa 304 huku visa vya maafa kutokana na virusi hivyo vikifika 10 tangu kuzuka kwa ugonjwa huo,” alisema Bashey.
Naibu huyo wa mkurugenzi wa huduma za matibabu alisema kuwa idadi ya sampuli zilizopimwa tangu kuzuka kwa virusi hivyo ni 3,876.
Eneo la Garissa mjini linaongoza kwa visa 238,likifuatiwa na Dadaab kwa visa 51, Fafi 13 huku Lagdera na Hulugho zikinakili kisa kimoja kila moja.
Ijara na Balambala hazijanakili kisa chochote.
Hata hivyo Bashey alidokeza kuwa wahudumu wa afya wako katika hatari ya kuambukizwa covid-19 akisema kuwa kati ya wahudumu 497 wa afya waliopimwa virusi hivyo, 45 walithibitishwa kuambukizwa.
Alisikitikia idadi kubwa ya wagonjwa wanaotoroka vituo vya kuwatenga waathiriwa wa Covid-19 akisema wanahatarisha maisha ya wapendwa wao kuambukizwa virusi hivyo.