Kamanda wa polisi katika kaunti ya Machakos Issa Mohamud amewatahadharisha wakazi wa kaunti hiyo dhidi ya kukiuka masharti yaliyowekwa kukabiliana na janga la Covid-19 hasa wakati huu ambapo visa vya maambukizi ya virusi vya corona vinazidi kuongezeka nchini.
Mohamud alisema kuwa wengi wa wakazi wamegeukia mienendo ya awali na kukiuka kabisa masharti yaliyowekwa na wizara ya afya ya kudhibiti kusambaa kwa virusi vya corona.
Mohamud ambaye alikuwa akiwahutubia wanahabari Machakos alisema kuwa suluhu la kukabiliana na janga la corona ni kwa wananchi kuzingatia masharti yote ya afya kama vile kuto-tangamana kwa karibu, kuvaa barakoa, kunawa mikono na kuepuka kuzurura zurura.
Alionya kuwa polisi watawakamata wote watakaopatikana wakikiuka sharia za afya za serikali za kudhibiti kusambaa kwa virusi hivyo katika kaunti hiyo.
“Kila mmoja anapaswa kuzingatia kikamilifu masharti yaliyowekwa na wizara ya afya kwa nia ya kujikinga dhidi ya virusi hivyo na wala sio kwa sababu ya maafisa wa usalama. Watu wanafariki kutokana na ugonjwa huu na ni nidhamu tu ambayo itatuokoa,”alisema afisa huyo.
Juma lililopita afisa wa afya katika kaunti ndogo ya Mwala Dkt Danson Muya aliwashauri wananchi kutembelea taasisi zilizoidhinishwa za afya ili kukaguliwa hali zao za afya pindi tu wanapoanza kuhisi dalili za homa kama njia ya tahadhari ya kukabiliana na maradhi ya Covid-19.
Kulingana na daktari Muya, kaunti ndogo ya Mwala imewapoteza watu watano kutokana na covid-19, tangu ugonjwa huo uripotiwe hapa nchini kwa mara ya kwanza mwezi Machi.